Winga wa Tanzania Prisons, Zabona Hamis atakuwa nje ya uwanja kwa zaidi ya miezi miwili baada ya kubainika kuumia fuvu la kichwa kufuatia ajali ya pikipiki aliyoipata tangu mechi yao na Ihefu, Januari 21 mkoani Mbeya
Nyota huyo aliyewahi kuichezea Alliance FC kwa mafanikio alijiunga na Prisons mapema msimu huu na katika mechi za karibuni amekuwa na mchango mkubwa kikosini.
Ofisa habari wa timu hiyo, Jakson Mwafulango amesema nyota huyo alipata ajali tangu walipomaliza mchezo wao na Ihefu na taarifa za daktari wa klabu, Kilulu Masonga ni kuwa alibainika kuumia fuvu la kichwa
Amesema kwa sasa staa huyo tayari amewasili Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu zaidi na wanatarajia mchezaji huyo atarejea uwanjani akiwa salama baada ya kipindi hicho
"Alikuwa anatoka kambini anavuka barabara kwenda dukani ndio akagongwa na pikipiki, lakini uongozi upo karibu naye kuhakikisha anapata matibabu na jana amepanda ndege kwenda Dar es Salaam," alisema Mwafulango