Simba yazindua kampeni ya ushindi Tegeta

Joel JJ By Joel JJ β€’ 15th February 2023


Simba yazindua kampeni ya ushindi Tegeta

Mwenyekiti wa klabu ya Simba Murtaza Mangungu amewataka mashabiki wa timu hiyo kuujaza uwanja wa Benjamin Mkapa katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Raja Casablanca ambao utapiwa Jumamosi, Februari 18

Akizungumza Tegeta leo katika tukio la uzinduzi wa hamasa kuelekea mchezo huo, Mangungu alisema hamasa ni kubwa kwa wachezaji na wameahidi watashinda mchezo huo wanachohitaji ni kuwaona mashabiki wao kwa wingi uwanjani

"Dhumuni letu (viongozi) tunataka uwanja ujae. Kwa namna tulivyozungumza na wachezaji na benchi ka ufundi wako tayari kutupa ushindi"

"Tunamshukuru Mhe. Rais kwa ahadi ya fedha. Nikiwa mwakilishi wenu napenda kuwambia wachezaji wamefurahi na tunamuahidi Mhe. Rais kuhakikisha tunashinda," alisema Mangungu

Nae Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema suala la ushindi kwenye mchezo dhidi ya Raja Casablanca sio mjadala lakini muhimu ni mashabiki kujitokeza kwa wingi kujaza uwanja wa Mkapa ili kuwapa hamasa wachezaji

"Tunataka Jumamosi tushinde, lakini ili kufanikisha jambo letu kwa urahisi tunatakiwa tuujaze uwanja. Tunakwenda kuwalipia kisasi ndugu zetu waliokula bao 6, kama Taifa hatuwezi kukubali jambo hilo liendelee. Tunakwenda kuwaonyesha sisi sio vilaza, sisi ni Simba Sports Club"

"Hii ni mechi ya kihistoria, tukijaa mashabiki 60,000 hakuna namna ya Raja AC kutoka," alisema Ahmed


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.