Juzi baada ya mchezo wa kombe la Shirikisho kati ya Yanga dhidi ya TP Mazembe uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa na Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 3-1, Rais wa Yanga Injinia Hersi Said alionekana akiteta na winga hatari wa TP Mazembe Fellipe Kinzumbi
Kinzumbi anayetumia mguu wa kushoto alikuwa mwiba kwa safu ya ulinzi ya Yanga kwani ndiye mchezaji aliyeonekana kuisumbua ngome ya Yanga iliyokuwa chini ya nahodha Bakari Nondo Mwamnyeto
Baada ya mchezo, Hersi alionekana akimpongeza nyota huyo mwenye umri wa miaka 23 lakini pia akawa na mazungumzo nae ya faragha kwa muda mfupi
Moja ya mkakati wa Yanga kuelekea msimu ujao ni kuimarisha safu yake ya mawinga ambayo msimu huu imekuwa haina nguvu kubwa
Hersi anafahamika kwa kuwa na ushawishi mkubwa kwa wachezaji kutoka DR Congo, mpaka sasa Yanga ikiwa na wachezaji sita kutoka nchini humo
Mwanzoni mwa msimu huu Kinzumbi alikuwa na mgogoro na mabosi wake TP Mazembe akiwatuhumu kutaka kuongeza muda wa mkataba wake pasipo makubaliano



