Klabu ya Simba imekiri kupungua kwa ubora wa baadhi ya wachezaji wake kutokana na kucheza michuano ya kimataifa na Ligi Kuu kwa muda mrefu bila kupumzika
Meneja Habari na Mawasiliano ya klabu hiyo, Ahmed Ally, amesema kuna baadhi ya wachezaji wa timu hiyo wamefanya kazi kubwa kwa miaka mitano mfululizo kwenye michuano ya kimataifa, Ligi Kuu na michuano mingine, hivyo kama binadamu hawawezi kuwa na uwezo, kiwango au ubora ule ule waliokuwa nao awali.
"Simba imepungua ubora kidogo, lazima tuwe wa kweli. Kwanza kuna nyota wetu ambao ubora wao umepungua kidogo kwa sababu ya kuchoka, wamefanya kazi kubwa kwa miaka mitano, wamecheza sana kwa miaka yote hiyo michuano ya kimataifa, Ligi Kuu na michuano mingine mfululizo"
"Hakuna binadamu ambaye anaweza kukupa asilimia 100 kwa miaka mitano, Mungu hajamuumba binadamu wa hivyo. Na unafahamu mpira kazi ya nguvu na kutumia akili na muda, unapocheza inatakiwa akili yako ifanye kazi kwa haraka sana, ukifanya kazi hiyo kwa miaka hiyo mfululizo lazima utachoka na kiwango kinapungua, ndiyo maana unaona ubora huo umepungua kwa sasa," alisema Ahmed.
Akatoa mfano mchezaji kama Mohamed Hussein 'Tshabalala', ambaye anacheza hatua ya awali ya michuano ya kimataifa, hatua ya kwanza, mechi sita za makundi na robo fainali kwa miaka mitatu, haiwezekani baada ya hapo atakuwa kwenye kiwango kile kile, ni lazima kitapungua kidogo.
Mbali na hilo alisema wapo baadhi ya wachezaji ambao walikuwa bora, lakini wameondoka kwenye klabu hiyo kwa kuuzwa.
"Kingine ambacho unaweza kuona ubora huo umepungua kidogo kwenye timu yetu, wapo watu wameondoka kwenye timu yetu, ama wameuzwa, au viwango vyao vilipungua, wakauzwa"