Baada ya kuvuna pointi tatu ugenini dhidi ya Vipers, Kocha Mkuu wa Simba, Robertiho Oliveira, ametambia mfumo mpya kuwasaidia kuibuka na ushindi huku akieleza matokeo hayo yamerudisha uhai mpya katika mipango yao ya kusaka pointi sita za michezo miwili ya nyumbani
Robertinho ameeleza kufurahishwa na kiwango kizuri cha wachezaji katika mchezo wa tatu wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Vipers na kufanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 Uwanja wa St Mary's, Uganda
Bao pekee la Simba lilifungwa na beki Henock Inonga baada ya mpira wa faulo uliopigwa na Mohamed Hussein 'Tshabalala' na kuchezwa kwa kichwa na Sadio Kanoute kisha Moses Phiri kabla ya mfungaji kuuzamisha nyavuni.
Akizungumza jana baada ya kurejea kutoka Uganda, Robertinho alisema kilichomfurahisha ni jinsi walivyocheza kitimu hasa kipindi cha pili huku muunganiko wa wachezaji vijana na wazoefu ukiwa mzuri.
"Wiki yote nilikuwa na kazi ya kubadilisha mfumo wa uchezaji na umeniletea matokeo chanya, nilijua timu yangu ya zamani ina wachezaji wazuri sana, wanacheza mfumo wa 4-3-3 na mimi nimetumia 4-4-2, lakini nimetumia wachezaji vijana kushambulia kama Kibu, Moses Phiri, tumefunga bao moja na kupoteza nafasi mbili ndani ya eneo la hatari, na nimejaribu kuchanganya wachezaji wazoefu na damu changa," alisema kocha huyo
Robertinho alisema jambo jema kwao ni kupata matokeo mazuri katika mchezo muhimu na kurejea nyumbani na pointi tatu bila kujali wameshinda bao ngapi.
"Katika Ligi ya Mabingwa hasa hatua ya makundi ushindi ndio jambo linalotakiwa, iwe moja, mbili au nne kinachoangaliwa ni pointi tatu.
"Tumecheza vizuri, tulikuwa na muunganiko mzuri mbinu yetu ilikuwa kuhakikisha tunapata ushindi kipindi cha pili muunganiko wetu uliimarika, kasi iliongezeka iliyochangiwa na wachezaji vijana na wazoefu," alisema Robertinho.
"Wachezaji wamepambana kwa kucheza kufa kupona katika mchezo ngumu na ushindani mkubwa ambao matokea hayo yametufanya tufufue matumain kuelekea katika michezo miwili inayofuata tukihitaji alama sita"