Yanga imetinga robo fainali ya michuano ya kombe la Shirikisho la Azam (ASFC) baada ya ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya Tanzania Prisons katika mchezo ulipigwa uwanja wa Azam Complex
Ulikuwa mchezo uliotawaliwa na Yanga kwa muda mwingi lakini hadi mapumziko hakukuwa na mabao kutoka kila upande licha ya Yanga kufanya majaribio mengi zaidi kwenye lango la Prisons
Hata hivyo Yanga ilirejea ikiwa na kasi zaidi kwenye kipindi cha pili, alikuwa nahodha Bakari Nondo Mwamnyeto aliyeitanguliza Yanga kwa bao la mapema kwenye kipindi cha pili kabla ya Jumanne Elifadhili hajasawazisha kupitia mpira wa kichwa
Kuingia kwa bao hilo kuiifanya Yanga iongeze kasi ya mashambulizi na kufanikiwa kufunga mabao mengine matatu kupitia kwa Clement Mzize aliyefunga mabao mawili pamoja na Stephane Aziz Ki aliyefunga kupitia mkwaju wa penati
Mzize angeondoka na mpira leo kama angefunga mkwaju wa penati kwenye dakika za majeruhi
Mzize anaongoza mbio za ufungaji bora akiwa amefikisha mabao sita
Mchezo huo ulishuhudiwa na Mwenyekiti wa Makampuni ya GSM, Ghalib Said Mohammed
Aidha klabu ya Singida Bi Stars imetinga robo fainali baada ya ushindi wa bao 1-0 dhidi ya JKT Tanzania wakati Geita Gold nao wakitinga robo fainali kwa ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Green Worriors



