Chelsea yatinga robo fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya

Joel JJ By Joel JJ β€’ 8th March 2023


Chelsea yatinga robo fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya

Ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Borrusia Dortmund usiku wa kuamkia leo, umeishuhudia Chelsea ikitinga robo fainali ya michuano ya ligi ya mabingwa barani Ulaya

Chelsea imetinga hatua hiyo kwa ushindi wa jumla wa mabao 2-1 ikipoteza kwa bao 1-0 kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa Ujerumani

Mfunzi wa Chelsea Graham Potter alifurahia usiku wake mzuri zaidi kama meneja wa Chelsea wakiitupa nje Borussia Dortmund na kutinga robo fainali ya Ligi ya Mabingwa.

Potter alikuwa chini ya shinikizo kubwa baada ya matokeo mabaya kufuatia gharama kubwa ya Chelsea kwenye soko la usajili, lakini ni wazi amepata matumaini mapya baada ya kuishuhudia timu yake ikicheza vyema dimba la Stamford Bridge.

Chelsea walistahili ushindi huo, ingawa walipoteza nafasi kadhaa kubwa kabla ya Raheem Sterling kufunga bao baada ya dakika 43, akimchambua kipa wa Dortmund Alexander Meyer baada ya kufumua shuti kali.

Bao hilo lilifanya matokeo yawe 1-1 kwa kuzingatia matokeo ya mechi ya kwanza ambayo Dortmund walishinda

Bao la pili lililoihakikishia Chelsea kutinga robo fainali lilitokana na mkwaju wa penati dakika ya 53 Kai Havertz akifunga baada ya kurudia pigo hilo mara mbili

Dortmund walilalamikia mazingira ya mkwaju huo kurudiwa lakini ilikuwa furaha kwa mashabiki wa Chelsea

Akizungumza baada ya mchezo huo, Potter alisema vijana wake walicheza vizuri na ushindi huo utawaongezea morali ya kufanya vizuri katika mechi zijazo

Katika mechi nyingine iliyopigwa jana, Benfica imetinga robo fainali kibabe kwa ushindi wa jumla wa mabao 7-1 dhidi ya Club Brugge

Jana Benfica waliibuka na ushindi wa mabao 5-1 wakiwa pia wameshinda mabao 2-0 katika mchezo wa kwanza

Leo mechi mbili zinapigwa Bayern Munich inaumana na PSG wakati Tottenham Hotspurs ikiikabili AC Milan

Bayern ina faida ya ushindi wa bao 1-0 walioshinda ugenini Ufaransa wakati Ac Milan nao walishinda bao 1-0 mechi ya kwanza nyumbani


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.