Kiungo wa Juventus, Paul Pogba anatarajiwa kuwa nje kwa angalau wiki tatu baada ya kuumia
Pogba (29) atakosa nafasi ya kujumishwa kwenye kikosi cha Ufaransa kwa ajili ya kuwania kufuzu kwa Euro 2024.
Pogba hakujumuishwa kwenye kikosi cha Juventus kilichocheza na Freiburg wiki iliyopita, pia alikosa mechi ya ushindi wa 4-2 dhidi ya Sampdoria Jumapili
"Leo asubuhi Pogba alikuwa akipiga faulo akahisi maumivu katika paja lake," kocha wa Juve Massimiliano Allegri alisema baada ya mechi ya Jumapili
Taarifa ya klabu ilisema kuwa Pogba alifanyiwa vipimo vya afya siku ya Jumatatu na kwamba amepata majeraha kidogo kwenye paja lake la mguu wa kulia
"Tayari ameanza mchakato wa matibabu ili kuhakikisha anarejea haraka katika majukumu yake," aliongeza Allegri
Juventus wana mchezo wa marudiano dhidi ya Freiburg siku ya Alhamisi, huku Pogba akikosa mchezo wa kwanza baada ya kuchelewa kuungana na timu Jumatano iliyopita
Pogba amecheza mechi mbili pekee akitokea benchi tangu ajiunge tena na Juve kutoka Manchester United msimu uliopita wa joto, huku mechi ya kwanza akicheza Februari 28.



