Kiungo mshambuliaji Feisal Salum 'Fei Toto', ni miongoni mwa wachezaji 31 walioitwa kwenye kikosi cha Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars kwa ajili ya kujiandaa na mechi mbili dhidi ya Uganda za kusaka nafasi ya kufuzu fainali za AFCON 2024 zitakazofanyika Januari hadi Februari mwakani
Fei Toto, ameitwa kwenye timu ya taifa akiwa hayupo kwenye kikosi cha Yanga kinachocheza Ligi Kuu na michuano ya Kombe la Shirikisho barani Afrika, na hivi karibuni akiwa amewasilisha barua kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini (TFF), kuomba kuvunja mkataba na klabu yake hiyo.
Awali, Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji ya TFF ilitangaza kuwa Fei Toto ni mchezaji halali wa Yanga, baada ya kutokea mgogoro wa kimkataba baina ya pande zote, ulioanza mwishoni mwa mwaka jana.
Mbali na mchezaji huyo, ambaye hajaonekana uwanjani kwa muda mrefu sasa, taarifa iliyotolewa jana na Idara ya Habari na Mawasiliano ya TFF chini ya Cliford Ndimbo, iliwataja wachezaji waliochaguliwa kujiunga na kikosi hicho ni Aishi Manula, Beno Kakolanya, Mzamiru Yassin kutoka Simba, Metacha Mnata, Kibwana Shomari, Fei Toto, Dickson Job, Bakari Mwanyeto, Mudathir Yahaya na Ibrahi Baka kutoka Yanga.
Wengine ni Datius Peter, David Luhende, Anuary Jabir na Abdallah Mfuko kutoka Kagera Sugar, Yahaya Mbegu kutoka Ihefu, Yasuph Kagoma wa Singida Big Stars, Sospeter Bajana na Abdul Suleiman 'Sopu' wa Azam FC, Edmund John wa Geita Gold, na Khalid Habibu wa KMKM.
Wachezaji wa Kitanzania walioitwa wanaosakata soka la kulipwa nje ya nchi ni pamoja na nahodha Mbwana Samatta kutoka KRC Genk ya Ubelgiji, pamoja Kelvin John ambaye anaichezea klabu hiyo, Simon Msuva wa Al-Qadsiah ya Saudi Arabia, Ramadhani Makame wa Bodrumspor ya Uturuki, Novetus Dismas wa Zulte Waregem ya Ubelgiji, Alphonce Mabula wa FK Spartak Subotica ya Serbia, Ben Starkie anayeichezea Basford United FC ya Uingereza, Haji Mnoga wa Aldershot Town ya Uingereza, Ally Msengi wa Swallows ya Afrika Kusini, Himid Mao wa Ghazi El Mahala SC ya Misri na Said Khamis wa Al-Fujairah ya Falme za Kiarabu.
Kikosi hicho kitakuwa chini ya Kocha Mkuu Adel Amrouche raia wa Algeria aliyetangazwa hivi karibuni, na kupewa jukumu la kukinoa kikosi cha Taifa Stars.