Simba, MobiAd zaingia makubaliano kukuza soka la vijana

Joel JJ By Joel JJ β€’ 23rd March 2023


Simba, MobiAd zaingia makubaliano kukuza soka la vijana

Klabu ya Simba leo imeingia mkataba wa miaka miwili na kampuni ya MobiAd kama wadhamini wakuu wa timu za vijana. Mkataba huo una thamani ya Tsh Milioni 500

Akizungumza katika hafla ya kusainiwa makubaliano hayo iliyofanyika Serena Hotel jijini Dar es salaam mapema leo, Mtendaji Mkuu wa Simba Imani Kajula alisema Simba inakwenda kutambia vipaji, kisha kuviendeleza kwa manufaa ya klabu na Taifa kwa ujumla

"Simba inakwenda mbele kutambua vipaji, kuvichukua na kuviendeleza na kuweza kutengeneza timu yenye vipaji vikubwa sana. Tunaamini Simba imara yenye vipaji haitaisaidia Simba pekee bali hata taifa letu"

"Yawezekana wachezaji tunaowaona ni sababu ya bahati, lakini tunatengeneza mfumo ambao kila kijana mwenye kipaji tutamwezesha kukuza kipaji chake, lakini sio tu kuendeleza kipaji cha mpira lakini pia kusoma shule"

"Leo tupo kwenye historia nyingine ya kuendeleza soka la vijana Tanzania. Mfumo wetu utakuwa mfumo wa wazi na endelevu," alisema Kajula

Mwekezaji wa klabu ya Simba Bilionea Mohammed Dewji 'Mo' anatarajiwa kuanzisha Academy ambayo ujenzi wake utaanza hivi karibuni

Rumisho Shikonyi ambaye ni Mtendaji Mkuu wa MobiAd amesema wanaamini maandalizi ya Taifa la kesho yanapaswa kuanza sasa

"Vijana ni taifa la kesho maandalizi yanaanza leo, kwa maana hiyo lazima tuunganishe nguvu. Tumeona hii ni fursa kuungana kwenye hii safari. Tunatangaza udhamini kwa timu ya vijana ya Simba Sports Club kwa mkataba wenye thamani ya Tsh. 500 milioni kwa miaka miwili," alisema Shikonyi

Mradi huo umepewa jila THE FUTURE IS NOW


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.