Mwenyekiti wa Chama cha Waamuzi Tanzania, Nassoro Hamdun, amesema wamejipanga kutoa semina tosha kwa waamuzi ili kuwaongezea ubora wao msimu ujao
Msimu wa 2022/23 wa Ligi Kuu Bara ambao umekuwa na ushindani mkubwa huku malalamiko kwa waamuzi yakiwa yamepungua kwa kiasi fulani, unatarajiwa kufikia tamati Mei 28, mwaka huu.
Hamdun amesema mafanikio ya ubora wa waamuzi msimu huu yametokana na umakini wa hali ya juu kuanzia Shirikisho la Soka nchini (TFF), Bodi ya Ligi (TPLB) na kamati ya waamuzi, hivyo wamepanga kuendeleza semina ili kuwaboresha zaidi waamuzi kuelekea msimu ujao wa 2023/24.
"Waamuzi wamekuwa bora msimu huu kutokana na umakini uliokuwapo kuanzia TFF, Bodi ya Ligi na Chama cha Waamuzi kwa kufuatilia mienendo yao ndani na nje ya uwanja ikiwa ni pamoja na kuwapa semina tosha za kuwataka wasimamie Sheria 17 za mchezo huo"
"Tumeandaa mikakati ya kuhakikisha waamuzi wetu wanakuwa bora zaidi msimu ujao na ili upate waamuzi walio bora kuchezesha soka ndani na nje ya nchi, wanatakiwa wapatiwe semina endelevu zitakazowasaidia kuwajenga ili kuwa imara," alisema



