Kikosi cha Singida Big Stars kimehitimisha kambi yake jijini Dodoma kwa ajili ya maandalizi ya mechi ya robo fainali ya Kombe la FA (ASFC), itakayochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Liti, mkoani Singida
Kocha Mkuu wa Singida Big Stars, Hans Van Pluijim, amesema kambi hiyo imewasaidia kuwajenga wachezaji wake na amepata nafasi ya kucheza mechi mbili za kirafiki.
"Tumekaa kambini kwa siku nane, nadhani sasa zinatosha kabisa kuivaa Mbeya City, tumecheza na mechi mbili za kirafiki ambazo zimetupa changamoto ya kutosha kuwarudisha wachezaji kwenye hali ya ushindani," alisema Pluijm.
Naye meneja wa timu hiyo, Nizar Khalfan, alisema waliitaji kujiimarisha kwa sababu watakutana na timu inayowapa ushindani kila wanapocheza.
"Tunawajua Mbeya City, siyo timu mbaya, tumecheza nao kwenye ligi, hatukuwa na mechi nyepesi nao, tunahitaji kusonga mbele ili tuchukue ubingwa wa FA, " alisema kiungo huyo wa zamani wa Yanga na Taifa Stars.



