Dean Smith ameteuliwa kuwa kocha wa Leicester City hadi mwisho wa msimu huu
Smith, 52, aliondoka Norwich mapema msimu huu baada ya kuzitumikia Aston Villa na Brentford
Leicester wako katika hatari ya kushuka daraja kufuatia kipigo cha nyumbani dhidi ya Bournemouth Jumamosi iliyopita. Wako pointi mbili kutoka kwa usalama zikiwa zimesalia mechi nane.
"Changamoto iliyo mbele yetu inaeleweka, lakini mimi na timu yangu ya kufundisha tumewahi kuipitia," Smith aliambia tovuti ya klabu.
"Kwa ubora katika kikosi hiki na idadi ya michezo iliyosalia, inawezekana sana"
Mchezo wa kwanza wa Smith kuinoa Leicester utakuwa ugenini dhidi ya mabingwa wa Ligi Kuu ya Uingereza Manchester City Jumamosi.
Craig Shakespeare anarudi King Power Stadium kama meneja msaidizi wa Smith.
Shakespeare alikuwa sehemu ya kikosi cha Claudio Ranieri wakati Leicester iliposhinda taji la Ligi Kuu ya Uingereza mwaka wa 2016.
Baadaye alichukua nafasi ya Mtaliano huyo kama meneja. Benchi la ufundi la Smith pia litajumuisha nahodha wa zamani wa Uingereza John Terry, ambaye alihudumu chini yake Aston Villa, pamoja na makocha wa sasa wa kikosi cha kwanza cha klabu hiyo Adam Sadler na Mike Stowell.