Klabu ya Yanga imemuahidi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh Dk Samia Suluhu Hassan kuwa wataendelea kupambana katika michuano ya kimataifa na ikiwezekana kufika hadi fainali kwa lengo la kuitangaza Tanzania
Hayo yalisemwa jana na Afisa Habari wa klabu hiyo, Ally Kamwe wakati akikabidhiwa kitita cha Sh Milioni 10 zilizotokana na ushindi wa mabao 2-0 ugenini katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa hatua ya robo fainali waKombe la Shirikisho dhidi ya Rivers United ya Nigeria
"Tuna mshukuru Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutekeleza ahadi ake kwa vitendo tumepokea pesa hizi na kiukweli zimetupa hamasa kubwa hadi kufika hapa sisi Yanga tunamuahidi kuipeperusha bendera ya nchi hii kwa kufika mbali ikiwezekana kubeba ubingwa wa Kombe la Shirikisho," alisema Kamwe
Yanga Jumapili hii itashuka uwanja wa Benjamin Mkapa kurudiana na Rivers United na inahitaji sare au ushindi wowote ili kuandika historia ya kutinga Nusu Fainali ya michuano hiyo kwa timu za Tanzania
Katika hatua nyingine, Kamwe amewataka mashabiki wa Yanga kununua tiketi kwa wingi kuhakikisha wanaujaza uwanja wa Benjamin Mkapa siku ya Jumapili katika mchezo wao dhidi ya Rivers United
Kamwe amesema ni nafasi adimu kwa mashabiki wa soka nchini kushuhudia historia ya aina yake ikiandikwa na klabu yao hivyo wanapaswa kwenda uwanjani kuwa sehemu ya kumbukumbu hiyo itakayodumu kwa miaka mingi



