Serikali yagharamia mashabiki 55 kuishangilia Yanga Afrika Kusini

Joel JJ By Joel JJ β€’ 14th May 2023


Serikali yagharamia mashabiki 55 kuishangilia Yanga Afrika Kusini

Serikali kupitia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo katika juhudi za hamasa kuendelea kuunga mkono michezo nchini hususani katika mashindano ya kimataifa, imegharamia jumla ya mashabiki 55 watakaosafiri kuelekea nchini Afrika Kusini, kwenda kuishangilia klabu ya Yanga

Ni katika mchezo wa pili wa hatua ya nusu fainali ya Kombe la Shirikisho Barani Afrika dhidi ya Marumo Gallants, utakaopigwa tarehe 17 Mei, 2023 kwenye uwanja wa Royal Bafokeng uliopo katika mji wa Rustenburg nchini humo

Hayo yalielezwa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Saidi Yakubu alipokuwa anazungumza na vyombo vya habari jana Mei 13, katika ukumbi wa uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam

Yakubu alisema msafara huo wa hamasa utaongozwa na Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Mheshimiwa Hamis Mwinjuma

"Katika hii safari, Serikali imesaidia Yanga kupeleka baadhi ya mashabiki 55 ambao wataondoka kesho (leo) jumapili tarehe 14 Mei, 2023 kueleka Afrika Kusini na huko wataungana na Watanzania waishio Afrika Kusini katika kuhakikisha wanatoa hamasa ya kutosha"

"Nimeongea na Balozi, wao pia wamejiandaa kuwapokea lakini pia wameandaa mabasi kutoka kila mji kuhakikisha Watanzania wanakuwa wengi katika mchezo huo,"alisema Yakubu.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa klabu ya Yanga, Andrew Ntime alisema kuwa wao kama timu wamejiandaa vizuri kuhakikisha wanapata matokeo mazuri kwenye mchezo huo huku akiishukuru serikali kutokana na mchango wake wa kupeleka mashabiki hao

Msafara wa Yanga umeondoka nchini Alfajiri ya leo Jumapili kuelekea Afrika Kusini kwa ajili ya mchezo huo utakaopigwa Jumatano


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.