Klabu ya Juventus imepata mapigo mawili usiku wa Jumatatu; kipigo cha 4-1 dhidi ya Empoli kwenye mchezo wao wa Serie A na lingine ni kukatwa alama 10 kufuatia uchunguzi wa mwaka mzima wa mikataba isiyofaa ya uhamisho
Mapema msimu huu Kibibi Kizee hicho cha Turin kilipokwa alama 15 kwa makosa ya kifedha na kutoa hesabu za uongo juu ya mikataba ya uhamisho hukumu ambayo ilienda sambamba na kusimamishwa baadhi ya viongozi wake wa zamani
Hata hivyo ilikata rufaa na kurejeshewa alama zote 15. Hukumu mpya imetangazwa Jumatatu Mei 22 ambapo safari hii Juventus wamepokwa alama 10 na kushuhudiwa ikiporomoka kwenye msimamo wa Serie A kutoka nafasi ya pili alama 69 mpaka nafasi ya 7 alama 59
Tofauti na kashfa ya 'Calciopoli', ambayo ilishuhudia Juventus wakishushwa daraja na kupokonywa mataji mawili ya Serie A mnamo 2006, hukumu hii ya sasa inahusiana makosa ya kifedha na ‘Plusvalenza’ (hesabu za uongo juu ya mikataba ya uhamisho) kimsingi ni kunufaika kutokana na mauzo ya mchezaji kutoka klabu moja hadi nyingine bila kufichua hesabu sahihi
Klabu ya AC imenufaika na maswaibu hayo ya Juventus katika mbio za kuwania kumaliza katika nafasi nne za juu. AC Milan ambayo weekend hii itachuana na Juventus wataingia katika mchezo huo wakiwa wamesogea mpaka nafasi ya nne kwenye jedwali la Serie A.



