Jioni ya leo macho na masikio ya Watanzania yataelekezwa uwanja wa Benjamin Mkapa kuwashuhudia Wananchi wakicheza fainali ya kombe la Shirikisho barani Afrika dhidi ya USM Alger
Ni mchezo wa mkondo wa kwanza ambao utapigwa saa 10 jioni wakati fainali ya pili itapigwa Algeria Ijumaa ijayo
Ni mechi ya kihistoria kwa Yanga na Tanzania kwa sababu hii ni mara ya kwanza mechi ya fainali ya michuano ya CAF inapigwa uwanja wa Benjamin Mkapa
Mwaka 1993 Simba walicheza fainali ya kombe la Washindi Afrika mchezo dhidi ya Stella Abidjan ukipigwa uwanja wa Uhuru (Shamba la Bibi) hivyo leo historia itaandikwa dimba la Mkapa kwa mechi ya fainali ya kombe la Shirikisho (CAF CC) kupigwa katika uwanja huo
Nafasi nadra kwa mashabiki kushuhudia mtanange huo wa kihistoria, ni wazi siti zote 60,000 zitakuwa na watu kwani tiketi zote za mchezo huo zimeuzwa
Yanga inawania taji kubwa la kwanza barani Afrika, leo inahitaji kushinda ili kujiweka katika nafasi nzuri ya kumaliza kazi ugenini kwenye mchezo wa pili
Yanga imepata maandalizi mazuri, kocha Nasreddine Nabi, wachezaji wamezungumza jinsi walivyo tayari kwa mchezo huo
Sapoti ya mashabiki hakuna shaka itakuwa kubwa lakini muhimu Wananchi wanapaswa kushangilia kwa muda wote wa mchezo ili kuhakikisha morali ya wachezaji wao haishuki
Wachezaji wa Yanga wanahitaji kufunga bao mapema ili kuvuruga mbinu za wapinzani wao ambao inafahamika mbinu watakayotumia zaidi leo ni kucheza kwa tahadhari pamoja na kupoteza muda
Mipira ya adhabu na kona inapaswa kudhibitiwa vyema kwani hiyo ndio itakuwa silaha kubwa ya USM Alger katika mchezo huo pamoja na kocha wao kudai hawakuja Tanzania kupaki basi
Hii ni siku ya kihistoria kwa Yanga na nchi kwa ujumla, matumaini ni kuona Yanga ikiibuka na ushindi mnono leo