Jana jiji la Dar es salaam lilisimama kwa saa kadhaa kupisha Tamasha kubwa la Michezo ukanda wa Afrika Mashariki na kati, SIMBA DAY
Ni rekodi juu ya rekodi kwa Simba, uwanja wa Benjamin Mkapa haukutosha kuwachukua watu wote waliojitokeza kushuhudia utambulisho wa kikosi cha Simba kwa ajili ya msimu wa 2023/24
Shamrashamra zikanogeshwa na ugeni wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk Samia Suluhu Hassan ambaye aliwapongeza Simba kwa kuandaa Tamasha hilo kubwa
Tamasha hilo lilihitimishwa na mchezo wa Kimataifa wa kirafiki kati ya Simba dhidi ya Power Dynamos, mabingwa wa Ligi Kuu ya Zambia
Simba ikabuka na ushindi wa mabao 2-0, Willy Onana na Fabrice Ngoma wakifunga mabao hayo yaliyohitimisha kilele cha furaha ya mashabiki wa Simba baada ya kuona ubora wa timu yao
Onana ndiye alianza kuwapa furaha mashabiki wa Simba baada ya kufunga bao la kuongoza kipindi cha kwanza lililodumu hadi mapumziko huku bao la pili likifungwa kipindi cha pili
Kipindi cha kwanza Simba walianza kwa kasi wakipasiana pasi fupi fupi na kuonana walionekana wakitumia winga za pembeni kutengeneza mashambulizi
Mashambulizi yao yalikuwa yanasukwa na Willy Onana na Clatous Chama ambao walikuwa wanacheza kwa kubadilishana upande
Onana alionekana kuwavutia zaidi mashabiki wa Simba kutokana na namna alivyokuwa anapiga pasi za uhakika kwa kufikisha kwa mtu sahihi. Dakika ya 45 za kipindi cha kwanza zilithibitisha ufundi wake baada ya kukwamisha mpira nyavuni na kuwanyanyua mashabiki lukuki waliojitokeza kwa Mkapa
Mchezaji mwingine aliyewavutia Wanasimba ni beki wa kati Che Fondoh Malone aliyeonekana kuwa mahiri katika ulinzi pamoja na kuanzisha mashambulizi



