Licha ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Asas Fc katika mchezo wa mkondo wa kwanza hatua ya awali ligi ya mabingwa barani Afrika, Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amesema hakuridhishwa na idadi ya mabao ambayo walifunga katika mchezo huo
Stephane Aziz Ki na Kennedy Musonda walifunga mabao ya Yanga katika mchezo uliopigwa uwanja wa Azam Complex, Chamazi Yanga ikitawala wakati wote
Gamondi amesema kipindi cha kwanza vijana wake hawakucheza katika ubora wao lakini kipindi cha pili walirejea wakiwa bora zaidi na pengine walistahili kufunga mabao zaidi ya matano
"Nimefurahi tumeshinda lakini sikuridhishwa na umakini katika matumizi ya nafasi. Kipindi cha kwanza hatukucheza vizuri sana lakini kipindi cha pili tulitawala mchezo kutengeneza nafasi nyingi. Pengine tulipaswa kufunga mabao matano hata sita"
"Wapinzani wetu hawakutaka kucheza mpira kwenye kipindi cha pili, zaidi walijiangusha na kutumia kila mbinu kutupunguza kasi, jambo muhimu tumeshinda"
"Tuna dakika nyingine 90 mwishoni mwa wiki nafikiri tunaweza kumaliza mchezo huu na kusonga mbele hatua inayofuata," alisema Gamondi
Gamondi amesema wataendelea kufanya maboresho katika safu ya ushambuliaji ili kuhakikisha wanatumia vyema nafasi wanazotengeneza



