Kiungo wa Singida Fountain Gate kutoka Brazili, Bruno Gomes amesema ana kazi kubwa ya kufanya kurudisha ubora wake wa msimu uliopita baada ya kukiri kuchelewa kujiunga na timu kumemrudisha nyuma kiasi kwamba hadi sasa bado anajitafuta
Bruno aliyekuwa kinara wa mabao wa Singida BS msimu uliopita akifunga mabao 10, alienda kuoa kwao Brazili na alichelewa kujiunga na kambi ya maandalizi ya msimu mpya na kujikuta akishindwa kutumika kwenye mechi zote ilizocheza timu hiyo kuanzia zile za kirafiki za kimataifa hadi mechi ya CAF
Bruno amekiri ana kazi kubwa ya kujitafuta hadi ajipate kurejea kwenye makali aliyokuwa nayo katika msimu wa kwanza na kikosi hicho cha Big Stars
"Nimejiunga na timu kwa kuchelewa bado sipo imara zaidi, lakini naamini hilo haliwezi kuniondoa mchezoni naamini nina muda na nafasi ya kuonyesha kile nilichonacho. Usajili uliofanyika unaniongeza changamoto ya kupambana zaidi na utanipa nguvu ya kuniongezea ubora kutokana na kuhitaji nafasi ya kucheza kikosi cha kwanza," Bruno alinukuliwa na Mwanaspoti



