Daktari wa Mtibwa Sugar, Lawrance Mushi amesema hali ya mlinda lango Mohamed Makaka imeimarika na tayari ameruhusiwa kutoka Hospital ya General mkoani Dodoma alikokuwa amelazwa
Makaka alishindwa kuendelea na mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Dodoma Jiji uliomalizika kwa sare ya bao 1-1 katika dakika ya 25 tu baada ya kuanguka ghafla na nafasi yake kuchukuliwa na Razack Shekimweri.
"Alianguka ghafla bila ya mpira wowote wa kugombania na mchezaji na baada ya kumuangalia ili kumpatia huduma ya kwanza uwanjani nikagundua alipoteza fahamu, hivyo tukamuwahisha hospitali," alisema
Taarifa iliyotolewa na Mtibwa Sugar jana, ilibainisha kuwa Makaka ameruhusiwa kutoka hospitalini baada ya afya yake kuimarika
"Hali ya Mohamed Makaka imeimarika na tayari karuhusiwa kutoka hospitalini, tunawashukuru wote mlioshirikiana nasi katika kipindi cha tatizo hilo hili," ilisema taarifa ya Mtibwa



