Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amesema kikosi chake kimejipanga kushinda mchezo wa ligi kuu dhidi ya Ihefu Fc ambao utapigwa kesho Jumatano katika uwanja wa Highlands Estate huko Mbarali
Yanga ilitua Mbeya usiku wa kuamkia leo kuelekea mchezo huo wa raundi ya nne, Wananchi wana kumbukumbu ya kupoteza alama zote tatu msimu uliopita katika mchezo uliopigwa hapo Highlands Estate
Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari mapema leo, Gamondi alisema licha ya timu yake kutopata muda wa kujiandaa na mchezo huo, wako tayari na watapambana kuhakikisha wanashinda
"Tunashukuru tumefika salama Mbeya, hatukuweza kupata muda mzuri wa kujiandaa kama mnavyojua tumetoka kucheza mchezo wa Kimataifa Jumamosi"
"Tunajua umuhimu wa mchezo wa kesho dhidi ya Ihefu na tutafanya kila jitihada kuhakikisha tunapata matokeo mazuri kwenye mchezo huu," alisema Gamondi
Gamondi amesema licha ya baadhi ya wachezaji kuwa na majeraha, mazoezi ya mwisho leo yatampa nafasi ya kuamua mchezaji gani atamtumia katika kikosi chake hapo kesho
"Wachezaji wako kwenye hali nzuri na morali yao iko juu, kuna baadhi ya wachezaji wana majeraha lakini tutajua kwenye mazoezi ya mwisho leo jioni ni wachezaji wapi watakuwa sawa kwa ajili ya mchezo wa kesho"
"Tunafahamu kwamba ni mwanzo wa ligi na kila timu iko kwenye nafasi nzuri na kujaribu kufanya vizuri zaidi inapokutana na bingwa mtetezi, ni sisi sasa kuhakikisha tunaendelea kucheza kwa kiwango cha juu na nina imani tutaendelea kufanya hivyo ikiwa ni pamoja na kufanya vizuri kwenye mchezo wa kesho"
Yanga ndio vinara wa ligi kuu ya NBC baada ya kushinda mechi zote tatu za mwanzo, ni wazi Wananchi watazihitaji alama tatu hapo kesho ili kuhakikisha wanaendelea kusalia kileleni mwa msimamo wa ligi



