Wakati klabu ya Ihefu na Kocha Zuberi Katwila wakithibitisha kufikia tamati kwa mkataba baina yao kwa makubaliano binafsi, imeelezwa kuwa kocha huyo anaenda kujiunga na Singida Big Stars kama kocha msaidizi
Katwila ni miongoni mwa makocha wanaotua Singida BS kusuka benchi jipya la ufundi litakaloongozwa na kocha wa kigeni ambaye atatangazwa hivi karibuni, huku timu hiyo ikiwa katika mpango wa kuachana na Mathias Lule na Thabo Senong waliokuwa wanaiongoza baada ya kuondoka kwa kocha mkuu Ernst Middendorp
"Kuna kocha kutoka Brazil anakuja kuchukua nafasi ya kocha mkuu na msaidizi wake atakuwa ni Zuberi Katwila. Mpango wa kumchukua Katwila ulianza muda mrefu, ndio maana tulianza kumchukua kocha wa makipa, Peter Manyika," kimefichua chanzo ndani ya Singida
Leo Jumamosi asubuhi Ihefu ilitangaza kuachana na Katwila aliyekuwa akiinoa kwa miaka mitatu tangu Oktoba 2020 alipojiunga akitokea Mtibwa Sugar, klabu aliyowahi kuichezea



