Mnyama Simba Sc ameunguruma uwanja wa Benjamin Mkapa akiendeleza rekodi ya ushindi kwa asilimia 100 msimu huu baada ya ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ihefu
Dhamira ya Simba kuusaka ubingwa imeendelea kudhihiri kwa wababe hao wa soka ukanda wa Afrika Mashariki kuendelea kushusha vipigo kwa kila anayekuja mbele
Haukuwa mchezo mwepesi kwa vijana wa Robertinho lakini suala la alama tatu ndio matokeo waliyohitaji na walifanikiwa kuyapata
Jean Baleke aliitanguliza Simba kwa kufunga bao la kwanza dakika ya 13 akitumia makosa ya safu ya ulinzi ya Ihefu Fc
Walima mpunga hao kutoka Mbarali wakarejea mchezo kwa kusawazisha bao kupitia kwa Ismail Juma kabla ya Moses Phiri hajaihakikishia Simba alama tatu muhimu ambazo zimewafanya wafikishe alama 18 sawa na Yanga lakini Simba ikiwa na mechi moja ya kiporo
Phiri ameendelea kuonyesha thamani yake licha ya kutopata muda mrefu wa kucheza. Phiri amefikisha mabao matatu msimu huu






