Baada ya mapumziko ya siku chache, kikosi cha Simba kimerejea mazoezini leo kuanza maandalizi ya mchezo wa kwanza wa hatua ya makundi ligi ya mabingwa barani Afrika dhidi ya Asec Mimosas
Mchezo huo utapigwa Novemba 25 katika uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam
Simba imerejea mazoezini ikiwa bado iko chini ya Kaimu Kocha Mkuu Daniel Cadena na Kocha Msaidizi Seleman Matola wakati mabosi wa Simba wakiendelea na mchakato wa kusaka kocha mpya
Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema wiki hii watamtambulisha Kocha Mpya ambaye atakuja na kocha msaidizi
"Tunakamilisha mchakato wa kupata kocha mpya, sio muda mrefu tutamtambulisha sambamba na kocha msaidizi. Tunatarajia ataiandaa timu kuelekea mchezo dhidi ya Asec Mimosas," alisema Ahmed
Simba imeweka malengo ya angalau kutinga nusu fainali ya ligi ya mabingwa ikiwa kundi B sambamba na Asec, Jwaneng na Wydad



