Kuelekea mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya Asec Mimosas utakaopigwa Novemba 25 katika uwanja wa Benjamin Mkapa, Simba imetangaza viingilio vya mchezo huo
Akizungumza katika Mkutano na Wanahabari, Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ally amesema wameweka viingilio rafiki ili kuhakikisha Wanamsimbazi wanajitokeza kwa wingi kuishangilia timu yao katika mchezo muhimu
"Leo tunazungumzia maandalizi ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya ASEC Mimosas. Utachezwa siku ya Novemba 25, 2023 saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa Mkapa. Wageni watawasili Novemba 23, 2023 wakiwa na msafara wa watu 31. Waamuzi wa mchezo watatoka nchini Misri."
"Viingilio vya mchezo huu ni; Mzunguko - Tsh. 5,000. VIP C - Tsh. 10,000. VIP B - Tsh. 20,000. VIP A - Tsh. 30,000 na Platinum - Tsh. 150,000"
"Wageni rasmi wa mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya ASEC Mimosas watakuwa ni mashabiki wa Simba. Kwanza wametoka kushinda tuzo ya mashabiki bora hivyo kila Mwanasimba akija siku hiyo ajue yeye ni mgeni rasmi."
"Tusahau yaliyopita na tuangalie mbele. Huu ni mchezo wa Ligi ya Mabingwa tukipoteza na tukiwa nyumbani hatutakuwa kwenye sehemu nzuri ya kwenda hatua ya mbele. Twendeni tukawape moyo wachezaji wetu kwamba tunaanguka pamoja na kusimama pamoja," alisema Ahmed
Ahmed amesema kikosi kinaendelea na mazoezi Mo Simba Arena kujiandaa na mchezo huo huku akibainisha kuwa uongozi uko katika hatua za mwisho kukamilisha mchakato wa kocha mpya
"Kikosi kipo mazoezini kuanzia siku ya Jumatatu. Mazoezi yanawahusu wachezaji wote ambao hawana majukumu ya timu za taifa. Ambao wapo kwenye timu za taifa watajiunga na wenzao wakitoka huko. Kikosi bado kipo chini ya Kocha Seleman Matola na Dani Cadena. Uongozi unaendelea na jitihada za kutafuta kocha mpya, mchakato utakamilika muda si mrefu"
"Tupo katikati ya mashindano lazima tutafute kocha ambaye yupo active, atakuwa tayari kuanza majukumu ili akifika kazi ianze"



