Kamati ya Uendeshaji na Usimamizi wa Ligi Kuu ya Bodi ya Ligi imemfungia kiungo wa Yanga Khalid Aucho mechi tatu kwa kosa la kumpiga kiwiko mchezaji wa Coastal Union Ibrahim Ajibu katika mchezo wa ligi kuu
Aucho pia ametozwa faini ya Tsh 500.000/- kutokana na tukio hilo ambalo pia aliadhibiwa uwanjani kwa kupewa kadi ya njano
Klabu ya Yanga imetozwa faini ya Tsh Milioni 5 kwa kosa la kuingia uwanjani kwa kupitia mlango usiokuwa rasmi kwenye mchezo dhidi ya Simba uliomalizika kwa Yanga kuibuka na ushindi wa ,mabao 5-1
Kocha Msaidizi Moussa Ndao na mlinda lango Digui Diarra wametozwa faini ya Tsh 500,000/- kutokana na makosa waliyofanya kwenye mchezo huo
Ndao alidaiwa kuwatolea lugha za matusi maafisa wa benchi la ufundi la klabu ya Simba wakati Diarra alidaiwa kushangilia mbele ya benchi la ufundi la Simba
Klabu ya Simba imetozwa faini ya Tsh Milioni 1 kwa kocha la wachezaji wake kuchelewa kutoka nje kwenye vyumba vya kuvalia nguo katika mchezo wa ligi kuu dhidi ya Yanga
Aidha wachezaji Kibu Denis na Hennock Inonga wametozwa faini ya Tsh 500,000/- kila mmoja wakidaiwa kushangilia bao la Simba kinyume na taratibu
Kibu aliyefunga bao la Simba, alishangilia mbele ya jukwaa la mashabiki wa Yanga huku akitumia ishara ya kuwaziba midomo huku Inonga akidaiwa kushangilia mbele ya benchi la ufundi la Yanga
kamati hiyo pia imewafungia miezi sita mashabiki wanne wa Simba wanaodaiwa kumshambulia shabiki wa Yanga kwenye mchezo wa ligi kuu dhidi ya Ihefu Fc






