Kuelekea mchezo wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Al Ahly ambao utapigwa Jumamosi Disemba 02, leo Yanga imefanya tukio la aina yake visiwani Zanzibar kwa kuzindua siku ya BACCA DAY
Akizungumza katika hafla maalum ya uzinduzi wa tukio hilo, Rais wa Yanga Injinia Hersi Said amesema ni mwendelezo wa utamaduni wa Yanga kuwapa thamani wachezaji wao lakini safari hii tukio hili limekwenda mbali zaidi kwa ajili ya manufaa ya nchi
"Tumekuwa na Maxi Day, Aziz Ki Day, wote walipata nafasi ya kutengenezewa thamani katika mechi zilizopita. Tumekutana hapa Zanzibar leo kwa ajili ya mchezaji wetu Ibrahim Bacca"
"Yanga ilimpa nafasi Bacca ya kuonyesha kipaji chake mazoezini na kwa utulivu na uvumilivu ilimchukua miezi kadhaa mpaka kuaminiwa kwenye kikosi cha kwanza"
"Leo tumekutana kuzindua Bacca Day ambayo kilele chake ni Disemba 02 pale uwanja wa Benjamin Mkapa katika mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya Al Ahly"
"Tukio hili limekwenda mbali zaidi sio tu kumpa thamani mchezaji wetu, Taasisi kubwa mbili hapa Zanzibar, ZRA na ZIPA zilipelekewa mapendekezo jinsi gani tukio hili linaweza kuwaongezea thamani"
"Taasisi hizo zimeweka fedha kwa ajili ya kudhamini Bacca Day kila Taasisi ikitoa Tsh Milioni 20. Nawapongeza ZIPA na ZRA kwa kuona kwa kiasi gani Bacca day inaweza kutumika kuwatangaza"
"Leo natangaza rasmi kuzindua Wiki ya Bacca Day ambayo kilele chake ni Disemba 02 pale uwanja wa Benjamin Mkapa," alisema Hersi
Nae Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Yanga Ali Kamwe amesema Disemba 02 itakuwa siku maalum hivyo watakuwa na mtoko maalum
"Kama una msuli wako uliuweka ndani kwa muda mrefu basi Jumamosi ndio siku yake. Vaa jezi yako na msuli wako njoo uwanjani"
"Lakini pia kama una kanzu yako basi vaa njoo nayo siku hiyo kuja kuipa thamani Bacca Day," alisema Kamwe



