Baada ya mechi tatu za hatua ya makundi kukamilika, Yanga imekumbana na matukio kutotendewa haki na waamuzi na hivyo kupeleka malalamiko kwa Shirikisho la soka barani Afrika (CAF) baada ya matukio yaliyojiri kwenye mchezo dhidi ya Medeama
Ukianza na mchezo dhidi CR Belouizdad waamuzi waliwapendelea wenyeji wazi wazi katika matukio mengi ikiwa ni pamoja na kuinyima Yanga mkwaju wa penati baada ya Pacome Zouzoua kuangushwa ndani ya eneo la hatari dakika za mwanzo katika mchezo huo
Kwenye mchezo dhidi ya Al Ahly ambao ulipigwa uwanja wa Benjamin Mkapa kulikuwa na matukio mengi ambayo mwamuzi alionekana kuwa na kigugumizi hasa inapoonekana faida ni kwa upande wa Yanga
Tukio la Pecy Tau kumkanyaga Joyce Lomalisa na kumsababishia maumivu yaliyomfanya ashindwe kuendelea na mchezo ni mfano wa matukio hayo. Mwamuzi hakutoa kadi yoyote katika tukio ambalo Tau angeweza hata kuonyeshwa kadi nyekundu
Mchezo uliofuata dhidi ya Medeama nao haukuwa na tofauti kwenye maamuzi. Achana na rafu mbaya aliyocheza beki Kwadwo Amoako dhidi ya Nickson Kibabage ambayo ilistahili kadi nyekundu ya moja kwa moja, katika mchezo huo Yanga ilinyimwa bao halali kabisa
Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga, Rodgers Gumbo amesema wamelazimika kuandika barua ya malalamiko kwa CAF wakimlalamikia yale waliyofanyiwa katika mchezo dhidi ya Medeama
"Ni kweli tumepeleka barua ya malalamiko kwa CAF kutokana na kuwa na ushahidi wa matukio ambayo ni wazi hatukutendewa haki ambayo ni pamoja na rafu ambayo mchezaji wetu Nickson Kibabge alichezewa na mchezaji wa Medeama ambaye alistahili kuonyeshwa kadi nyekundu lakini refa hakufanya hivyo"
"Lakini pia kuna tukio la bao letu halali ambalo Kibabage alifunga lakini refa akalikataa, tumejiridhisha lilikuwa bao halali"
"Tumewaandikia ili wajue nini cha kufanya kwa sababu matukio kama yale yananyima timu haki ya kupata ushindi na kuipa nyingine matokeo ambayo haijastahili," alisema Gumbo



