Baada ya kuiongoza Simba kwa takribani wiki mbili, Kocha Mkuu wa Simba Abdelhak Benchikha amesema kikosi chake kimesheheni wachezaji wengi wenye uwezo mkubwa lakini ipo changamoto katika baadhi ya maeneo hasa safu ya ushambuliaji
Benchikha amesema wanaendelea kufanyia kazi mapungufu hayo na anaamini baada ya muda kila kitu kitakuwa sawa
Benchikha amewasifu nyota wake wanaocheza eneo la kiungo kuwa wanafanya kazi kubwa na kwake ndio eneo lililomvutia zaidi
"Nafikiri tunakwenda vizuri, tuna timu yenye wachezaji wazuri lakini zipo changamoto katika baadhi ya maeneo"
"Nimeridhishwa na vile timu inavyocheza hasa eneo la kiungo, wanafanya kazi nzuri katika kuhakikisha kwamba wanakaba, lakini pia wanapiga pasi za uhakika kwenda mbele na wameonyesha jinsi gani wanataka kuona timu inapata ushindi"
"Ipo changamoto kidogo eneo la ushambuliaji, kwa sababu hatujafunga mabao mengi, ila nafanyia kazi hali hiyo na naamini baada ya muda kila kitu kitakaa sawa," alisema Benchikha
Nyota wanaon'gara katika eneo la kiungo ni Fabrice Ngoma na Sadio Kanoute ambao wamekuwa chaguo la kwanza tangu ujio wa Benchikha wakisaidiana na Mzamiru Yassin ambaye amekuwa akitumika katika kipindi cha pili
Simba imerejea Mo Simba Arena kujiandaa na mchezo unaofuata Ligi Kuu dhidi ya Kagera Sugar ambao utapigwa Ijumaa, Disemba 15 katika uwanja wa Uhuru