Burudani ya ligi kuu inaendelea uwanja wa Azam Complex leo wakati mabingwa watetezi Yanga watakapo wakaribisha Mtibwa Sugar katika mchezo utakaopigwa saa 12:30 jioni
Ni mchezo utakaozikutanisha timu zenye malengo tofauti, Yanga inahitaji ushindi ili kuisogelea Azam Fc ambayo iko kileleni mwa msimamo wa ligi kwa tofauti ya alama nne ikiwa imecheza mechi tatu zaidi
Mtibwa Sugar wanaburuza mkia wakishinda mechi moja tu msimu huu lakini timu hiyo inanolewa na Kocha Zubeir Katwila ambaye Wananchi wanamkumbuka kwani ndiye kocha pekee aliyepata ushindi dhidi ya Yanga msimu huu wakati akiinoa Ihefu Fc
Kwa Kocha Miguel Gamondi, huu ni mchezo muhimu kwa kikosi chake kushinda ili kuongeza morali kuelekea mchezo wa ligi ya mabingwa dhidi ya Medeama Fc utakaopigwa Jumatano, Disemba 20 katika uwanja wa Benjamin Mkapa
Kwenye makaratasi unaweza kuonekana ni mchezo mwepesi kwa Yanga lakini kiuhalisia haitakuwa mechi nyepesi
Kwa ubora ambao Yanga wameonyesha kwenye ligi msimu huu, kila timu inapocheza na Yanga inatamani kuingia kwenye rekodi ya kufanikiwa kuwazuia Wananchi kuibuka na ushindi
Hivyo ni mechi ambayo kwa Mtibwa Sugar itakuwa kama fainali wakati Yanga wao watahitaji kuendeleza ubabe wao kwenye ligi msimu huu



