Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amesema hawakuwa bora katika mchezo dhidi ya APR na hivyo kupoteza mchezo huo wa robo fainali ya Kombe la Mapinduzi kwa kufungwa mabao 3-1
Gamondi amesema walicheza vyema dakika 45 za kwanza lakini wakapoteza mwelekeo katika kipindi cha pili na kuwapa nafasi wapinzani wao kufunga mabao mepesi
Kocha huyo raia wa Argentina amesema licha ya kuondoshwa katika michuano hiyo, imemsaidia kubaini wachezaji ambao wana sifa ya kuendelea kuitumikia Yanga
"Tulikuwa bora katika kipindi cha kwanza lakini mwishoni tukafanya makosa ambayo yaliwapa nafasi APR kusawazisha"
"Kipindi cha pili tulipoteana, yawezekana ni uchovu au baadhi ya wachezaji kutokuwa katika daraja la ushindani sawa na wapinzani wetu"
"Timu yetu imewakosa wachezaji 14, wachezaji nane wamekwenda katika majukumu ya timu za Taifa na wengine wamekosekana kutokana na majeruhi na sababu nyingine"
"Lakini michuano hii imetusaidia kuwapa nafasi wachezaji wetu wa timu ya vijana na wengine ambao hawakutumika sana katika timu yetu ya kwanza"
"Pia imenisaidia kufanya tathmini juu ya uwezo wa baadhi ya wachezaji kuona kama wanastahili kuendelea nasi au la," alisema Gamondi



