Kocha Mkuu wa Yanga, Miguel Gamondi amesema kikosi chake kina nafasi ya kupata ushindi dhidi ya Mamelodi Sundowns na kutinga nusu fainali ya ligi ya mabingwa barani Afrika
Ukifuatilia mijadala mbalimbali hasa katika mitandao ya kijamii, utaona wengi wanaipa Yanga nafasi ndogo ya kuvuka mbele ya Mamelodi hata hivyo Gamondi anaamini hakuna jambo lisilowezekana kwa sababu ni wachezaji 11 kwa kila timu watakuwa uwanjani
Yanga itaikaribisha Mamelodi katika Uwanja wa Benjamin Mkapa March 30 na baada ya hapo timu hizo zitarudiana Aprili 5, mwaka huu, nchini Afrika Kusini na mshindi wa jumla atatinga nusu fainali
Gamondi aliyewahi kuinoa Mamelodi, amesema hana wasiwasi wowote kukabiliana na waajiri wake hao wa zamani akiamini wachezaji wake watakuwa tayari kukabiliana nao
"Muhimu kwetu ni kujipanga na kuweka juhudi, hatuna sababu ya kuhofia mchezo huu kwa sababu kila timu itakuwa na wachezaji 11 na dakika 90 zitachezwa nyumbani na ugenini"
"Jambo pekee ambalo linaweza kutusumbua kidogo ni uzoefu wa baadhi ya wachezaji katika michuano hii lakini pia naamini tunao wachezaji ambao wamecheza ngazi kama hii ya mashindano ambao uwepo wao utasaidia kuwajenga wale wengine, " alisema
Kwa miaka ya karibuni Mamelodi Sundowns imekuwa ikipata wapinzani kutoka Afrika Kaskazini katika hatua ya mtoano, mara ya mwisho kuwa na upinzani Kusini mwa Jangwa la Sahara ilikuwa msimu wa 2021/22 walipotupwa nje na Petro Atletico
Pengine hii inaweza kuwa nafasi pia kwa Yanga kuwaduwaza wababe hao wa soka la Afrika Kusini ambao wanasaka taji la pili la Ligi ya Mabingwa wakishinda taji hilo kwa mara ya mwisho mwaka 2016



