Licha ya maumivu makali ambayo Wanasimba wanapitia kutokana na mwenendo wa timu yao, Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Wekundu hao wa Msimbazi Ahmed Ally amewataka kuendelea kuwa uvumilivu kwani nyakati za furaha zinakuja
Juzi Simba ilipoteza mchezo wa pili msimu huu dhidi ya watani zao Yanga kwa kufungwa mabao 2-1 katika mchezo uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa
Ulikuwa mchezo wa tano mfululizo Simba inakosa ushindi katika michuano yote
Kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii, Ahmed amewapa Wanasimba ujumbe huu;
"Dhahabu hupitishwa kwenye moto mkali ili ipate thamani na iwe bora
Licha ya kuwa huteseka inapopita kwenye moto huo lakini mwishoe hubaki safi, bora na thamani yake huongezeka maradufu
Wana Simba tuvumilie kupita kwenye moto huu mkali ili tuwe bora na hadhi yetu irejee
Najua maumivu ni makubwa kwa kua moto mkali lakini hatuna budi kuvumilia kwani ndio njia pekee ya kurudi kwenye thamani yetu"
Kikosi cha Simba kinaelekea Zanzibar kushiriki Muungano Cup ambapo Jumatano itashuka uwanja wa New Amaan Complex kuikabili KVZ katika mchezo wa nusu fainali



