Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Yanga Ali Kamwe amewahakikishia Wanachama na Mashabiki wa timu hiyo kuwa msimu ujao wataendelea kuwaona wachezaji wao bora kikosini wakiwemo wale ambao mikataba yao inaelekea ukingoni
Wananchi bado hawana uhakika kama mchezaji wao bora wakati huu Stephane Aziz Ki na mlinda lango Djigui Diarra wataendelea kuwa sehemu ya kikosi hasa ikizingatiwa mikataba yao inamalizika mwishoni mwa msimu
Aziz Ki anatajwa kupokea ofa kutoka timu za hapa Tanzania, Afrika na hata nje ya Afrika, klabu zenye misuli ya pesa kama Mamelodi Sundowns na hata Al Ahly nazo zikitajwa kuiwinda saini yake
Kamwe amesema pamoja na mazingira hayo, anaamini Aziz Ki ataendelea kuitumikia Yanga kama ilivyo kwa wachezaji wengine ambao kocha Miguel Gamondi anahitaji kuendelea nao
"Aziz Ki ni kweli anamaliza mkataba wake lakini kwa hapa Tanzania sioni kama kuna timu ambayo anaweza kucheza tofauti na Yanga"
"Aziz anahitajika na timu nyingi, kwa hizi timu za Afrika Kusini Aziz hawezi kucheza na watu wanaofanya dhuluma namna ile"
"Ziko ofa nyingi lakini kubwa ambalo naweza kuwaambia wanayanga, wachezaji bora ambao wamewaona kwenye kikosi chetu wanasalia kwenye kikosi chetu," alisema Kamwe



