Msimu umemalizika, yasiyotarajiwa yametokea

Joel JJ By Joel JJ β€’ 29th May 2024


Msimu umemalizika, yasiyotarajiwa yametokea

Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2023/2024 imefikia tamati jana na kushuhudia Simba ikiambulia tiketi ya kushiriki michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika baada ya kumaliza kwenye nafasi ya tatu ikizidiwa idadi ya magoli na Azam ambao wataungana na Yanga kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika

Hii ni mara ya kwanza baada ya misimu sita kupita ikishiriki Ligi ya Mabingwa Afrika lakini sasa Simba italazimika kushiriki michuano hiyo namba mbili kwa ukubwa Afrika ikiungana na Coastal Union kuiwakilisha Tanzania kwenye michuano hiyo

Licha ya ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya JKT Tanzania kwenye mchezo wa mwisho, Uwanja wa Benjamini Mkapa, matokeo hayo yalizimwa na ushindi wa Azam FC wa mabao 2-0 dhidi ya Geita kwenye uwanja wa Nyankumbu mkoani Geita na kukata tiketi kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya misimu 10 kupita

Ushindi wa timu hizo umezifanya zote kumaliza msimu kwa kukusanya pointi 69 lakini Azam wakifaidika na uwiano mzuri wa magoli ya kufunga na kufungwa

Katika mchezo wa jana, Simba ilipata mabao yake kupitia kwa Saido Ntibazonkiza dakika mbili kabla ya mechi kumalizika kwa mkwaju wa penalti, na Willy Onana aliyeingia kipindi cha pili kuandika bao la pili kwenye dakika za nyongeza

Mkoani Geita, Azam Fc ilipata mabao yake kupitia kwa Yelson Mandoza dakika ya 58 na Feisal Salum 'Feitoto' dakika ya 71

Licha ya kufunga bao moja kwenye ushindi wa jana, Feitoto alishindwa kutwaa kiatu cha dhahabu cha ufungaji bora baada ya kuzidiwa na kiungo wa Yanga, Azizi Ki ambaye jana wakicheza na Tanzania Prisons kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, alifunga mabao matatu na kuisaidia timu yake kuondoka na ushindi wa mabao 4-1

Mabao hayo yamemfanya Aziz Ki kufikisha idadi ya mabao 21 akimuacha Feitoto kwa mabao mawili na kuongeza furaha kwa mashabiki wa Yanga ambao mapema wiki iliyopita walishuhudia timu yao ikitwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara kwa mara ya tatu mfululizo

Mchuano wa kuwania tuzo hiyo ulikuwa mkali na kabla ya michezo ya jana wachezaji wote walikuwa na magoli 18 na hivyo kusubiri michezo ya mwisho kujua nani atakuwa kinara wa mabao msimu huu

Mabao hayo matatu aliyofunga Aziz Ki yanamfanya kufikisha 'hat trick' mbili (mabao matatu katika mchezo mmoja) kwenye Ligi Kuu msimu huu ikitanguliwa na ile ya kwanza aliyoipata kwenye mchezo dhidi ya Azam, Oktoba 23, mwaka jana

Baada ya kukubali kipigo cha mabao 2-0 nyumbani dhidi ya Azam jana, Geita Gold inaungana na Mtibwa Sugar kushuka daraja moja kwa moja baada ya kumaliza kwenye nafasi ya 15 ikiwa na pointi 25 ambazo hazijaisaidia hata kucheza 'Play Off'

KT Tanzania baada ya kipigo dhidi ya Simba yenyewe imemaliza katika nafasi ya 13 ikiwa na pointi 32 na sasa itakwenda kucheza mechi ya mchujo dhidi ya Tabora United, ambayo nayo jana ilikutana na kipigo cha mabao 3-2 kutoka kwa Namungo FC kwenye uwanja wa Majaliwa, Ruangwa mkoani Lindi

Tabora United imemaliza ligi kwenye nafasi ya 14 ikiwa na pointi 27 na kujikuta ikicheza mchezo huo wa Play Off na JKT Tanzania

Mshindi wa jumla kwenye mchezo huo atakutana na Biashara United iliyoifunga Mbeya Kwanza kwenye michezo miwili ya Play Off kwa timu za 'Championship', mshindi wa jumla katika mechi hiyo atapata nafasi ya kucheza Ligi Kuu msimu ujao

IPP Media


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.