Klabu ya Yanga imesema kuwa baadhi ya mawakala wanaitumia klabu hiyo kwa ajili ya kuwapa thamani wachezaji wao na kuwauza kwa dau kubwa
Ofisa Habari wa klabu hiyo, Ali Kamwe, amesema baadhi ya Mawakala wa wachezaji wamekuwa na tabia ya kuwahusisha wachezaji kuwa wanatakiwa na Yanga ili kuzifanya timu zingine zipande dau wakati si kweli kama wanawahitaji
Kamwe alisema vitendo hivyo vilifanyika msimu uliopita na anashangaa msimu huu vimeibuka tena, akiwataka Mawakala kuwauza wachezaji kwa thamani zao halisi na kuacha kuitumia Yanga kwa njia ya kuwapandisha thamani na kupata pesa nyingi za usajili
"Mwaka jana hawa mawakala walitengeneza stori kuwa kuna mchezaji Yanga inamtaka, lakini alipokwenda klabu nyingine ikasemekana eti ameibiwa Uwanja wa Ndege, sisi wala hatukusema kitu," alisema Kamwe
Ingawa hakufafanua, lakini ukirejea moja ya stori za matukio ya msimu uliopita ilisemekana kuwa Simba ilimpora mchezaji raia wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Fabrice Ngoma, Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere, akiwa anakuja kusaini mkataba Klabu ya Yanga
"Kuelekea msimu unaokuja tunaanza kusikia tena habari kama zile, wanasema kuna kiungo tumepokonywa, si kweli ukiona hivyo hatukumhitaji, hivyo ni kazi ya Mawakala kupiganisha ili wapige pesa," alisema Ofisa Habari huyo.
Akizungumzia usajili, Kamwe alisema tayari wameshamaliza kazi iliyobaki ni kuwatangaza tu. Tangu awali, Yanga ilitangaza kuwa haitofanya usajili mkubwa sana kwani bado ina kikosi imara, na ilichofanya ni kuzuia wachezaji wake muhimu kubaki, na kufanya usajili wa wachezaji wachache tu wenye viwango vya hali ya juu kwa ajili ya kukiongezea nguvu kikosi
"Malengo tuliyonayo ni makubwa na usajili tulioufanya, watu watalia na kusaga meno," alisema Kamwe
Tetesi zinadai kuwa Yanga imekamilisha usajili wa wachezaji, Emmanuel Bola Lobota, winga kutoka Singida Black Stars, Agee Basiala, kiungo mshambuliaji kutoka AS Maniema Union na beki wa kushoto, Chadrack Boka kutoka Klabu ya Saint Eloi Lupopo, wote hao kutoka DR Congo
Mwingine ni kipa Khomein Abubakar wa Singida Black Stars, anayekwenda kuchukua nafasi ya Metacha Mnata, anayetajwa kuondoka