Serikali imesema kupatikana VAR ambayo itatumika kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao, kutapunguza malalamiko waliyokuwa wanatupiwa waamuzi kwa kile kilichokuwa kinaonekana hawafanyi maamuzi sahihi
Akizungumza jana kwenye hafla ya uzinduzi wa video ya usaidizi wa waamuzi maarufu kama VAR, uliofanyika kwenye Uwanja wa Banjamin Mkapa, Dar es Salaam, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, alisema kuwapo kwa kifaa hicho kitawezesha waamuzi kufanya maamuzi yao sahihi kwani watakuwa na uwezo wa kurudia kile ambacho watakuwa hawajakiona, ili timu ziweze kupata ushindi wa halali
Aidha, Waziri Majaliwa, alitaka viwanja ambavyo havina ubora, viwekwe pembeni kwani kuelekea msimu ujao wa Ligi Kuu, vitaharibu mvuto wa ligi yenyewe
"Nampongeza Rais Karia (Wallace) kwa juhudi kubwa tangu aanze kulisimamia Shirikisho la Mpira wa Miguu tumepata mafanikio makubwa kupitia mpira wa miguu, na kwa maboresho haya naamini Tanzania itapanda na kushika nafasi ya nne kwenye Ligi ya Afrika kutokana na uwekezaji huu," alisema Waziri Mkuu
Alisema serikali inalitaka Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), kuendelea kushirikiana na kampuni zilizowekeza kwenye utangazaji wa michezo mbalimbali nje na ndani ya nchi, ili kukuza soka la nchi na kulitangaza nje, pamoja na kuwaweka sokoni wachezaji wa Kitanzania.
Nae Rais wa TFF, Karia, alisema kuwa wameamua kubaki na idadi ya wachezaji 12 wa kigeni licha ya wadau wengi kutaka idadi hiyo ipunguzwe
Alisema sababu kuwa ni kwamba klabu za Tanzania zimepata mafanikio makubwa kwa miaka ya hivi karibuni kutokana na kuwa na wachezaji wa kigeni, ambapo kabla ya hapo zilikuwa hazifanyi vema
"Kwa takwimu tulizonazo wachezaji wa kigeni hawajafika 70 kati ya wachezaji 600 ambao huwa wanashiriki Ligi Kuu, hivyo wachezaji wetu wanatakiwa na wao watoke nje ili wakapate changamoto na siyo sisi kupunguza idadi ya wachezaji wa kigeni," alisema Rais Karia
Alisema wachezaji wa kigeni wameongeza ushindani kwenye Ligi Kuu na kuchangia kukua kwa viwango vya wachezaji wa ndani, kiasi cha kuisaidia timu ya taifa kufanya vizuri
"Tulipokuwa tukicheza na DR Congo na Zambia, wachezaji wengi wa Tanzania walikuwa wa ligi ya ndani na wadogo, lakini walifanya vizuri sana kiasi cha kushangaza wengi, kwa sababu hawana tena ule woga wa kuogopa wachezaji wa kigeni, kila siku wanacheza na wachezaji hao hao kwenye ligi au wapo timu moja, hiyo imetusaidia sana kama taifa," alisema



