Sakata la klabu ipi ina haki ya kummiliki beki Lameck Lawi, kati ya Simba na Coastal Union bado limebaki mikononi mwa Kamati ya Hadhi na Haki za Wachezaji iliyopo chini ya Shirikisho la Soka nchini (TFF), baada ya pande mbili jana kutoa maelezo mbele ya kamati hiyo, imeelezwa
Lawi msimu uliomalizika aliichezea Coastal Union na ulipomalizika akauzwa Klabu ya Simba, lakini wamiliki wake hao wa zamani walirejesha hela kwa madai muda waliowekeana wa malipo ulimalizika, jambo ambalo limezua mvutano kwani upande wa pili pia unasema ulifuata taratibu zote
Jana kila upande ulitoa ushahidi wake mbele ya kamati hiyo, Coastal Union, ikiwakilishwa na Katibu Mkuu wake, Omary Ayoub, huku Simba ikiwakilishwa na wanasheria wao
Kila timu imeendelea kushikilia msimamo wake ambapo Coastal Union wanadai wallirudisha fedha yote iliyotolewa na Simba baada ya kukiukwa kwa makubaliano baina ya pande mbili
Hata hiyo Simba imesisitiza mchakato huo ulikamilishwa kama walivyokubaliana, Coastal Union walipaswa kuwataarifu mapema kama kulikuwa na makubaliano yaliyokiukwa (suala la muda wa malipo)



