Morocco ataja siri ya ushindi wa Stars Ivory Coast

Joel JJ By Joel JJ β€’ 12th September 2024


Morocco ataja siri ya ushindi wa Stars Ivory Coast

Kocha wa Timu ya Taifa 'Taifa Stars', Hemed Morocco, amesema kujituma kwa wachezaji na kufuata maelekezo yake muda wote wa mchezo ndio sababu ya kuibuka na ushindi kwenye mchezo dhidi ya Guinea juzi usiku

Stars ikiwa ugenini juzi ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa 'kusisimua' wa mabao 2-1 na kuendelea kuweka hai na kukoleza mbio za kushiriki fainali za AFCON mwakani nchini Morocco.

Ushindi huo pia umepongezwa na Rais Samia Suluhu Hassan, ambapo kupitia ukurasa wake wa kijamii alisema;

"Hongera kwa vijana wetu wa Taifa Stars kwa ushindi mlioupata dhidi ya Guinea katika mchezo mlioucheza hapo jana (juzi)", alisema Rais Samia

Aidha, Rais Samia ameitakia mafanikio mema Taifa Stars katika michezo mingine iliyopo mbele yao ya kuwania kufuzu Fainali hizo za AFCON

Stars juzi iliingia kwenye mchezo huo huku ikiwa imetoka kubanwa mbavu nyumbani na Ethiopia waliowalazimisha kutoka suluhu kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa

Morocco amesema matokeo ya mchezo wao dhidi ya Ethiopia hayakuwafurahisha lakini yaliwaongezea morali ya kusaka ushindi kwenye mchezo wa juzi

"Baada ya mchezo na Ethiopia tulirudi kwenye uwanja wa mazoezi na kuanza kuyafanyia kazi mapungufu tuliyoyaona, lakini lazima niwapongeze wachezaji wangu kwa hali yao ya kujituma na kufuata maelekezo yote, hii ndio imepelekea tumepata ushindi huu muhimu," alisema Morocco

Alisema matokeo kwenye mchezo dhidi ya Ethiopia yaliwaumiza sana lakini wachezaji wake wameonyesha ukomavu mkubwa kwa kupambana dakika zote 90 kwenye mchezo wa juzi

"Japo niliamini kama tutapambana muda wote tunaweza kupata ushindi, sikutegemea wachezaji kujituma namna ile na kufuata maelekezo yangu kwa asilimia kubwa, ushindi huu umechochea morali kuelekea michezo inayofuata," alisema kocha huyo.

Magoli kwenye mchezo wa juzi yalifungwa na nyota wa Azam FC, Feisal Salum 'Feitoto' aliyefunga bao la kusawazisha baada ya awali Stars kutanguliwa kwa bao moja, goli la pili na la ushindi lilifungwa na kiungo mshambuliaji wa Yanga, Mudathir Yahaya

Matokeo hayo yameifanya Taifa Stars kushika nafasi ya pili kwenye kundi H wakiwa na pointi nne, pointi mbili nyuma ya vinara Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo huku Ethiopia wakishika nafasi ya tatu kwa kuwa na pointi moja na Guinea wanaburuza mkia kwa kutokuwa na pointi huku kila timu ikiwa imecheza michezo miwili

IPP Media


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.