Mshambuliaji Crispin Ngushi, amefunga bao lake la pili kwenye Ligi Kuu Tanzania, likiwa pekee katika mchezo ambao timu yake ya Mashujaa FC ilishinda 1-0 dhidi ya Coastal Union kwenye Uwanja wa KMC, Mwenge Dar es Salaam akisema lengo lake ni kufika mbali zaidi, hata kama itakuwa ni kurejea kwenye klabu yake ya zamani, Yanga
Ngushi, ambaye alijiunga na Mashujaa kwa mkataba wa mwaka mmoja, akitokea timu hiyo aliyoifunga Ijumaa iliyopita, Coastal Union ambako alikuwa akicheza kwa mkopo kutoka Yanga, alisema anashukuru kwa kupachika bao katika mchezo huo ambalo limekuwa la pili katika michezo mitatu tu aliyocheza akiahidi makubwa zaidi msimu huu
"Siri ni kwamba Mashujaa ninachokipata naridhika nacho, hata Yanga ilikuwa hivyo ila nilikuwa sipati sana muda wa kucheza kama huku, nitazidi kufanya mazoezi kwa bidii ili niweze kufunga zaidi, hata ikitokea timu yoyote kubwa inanitaka, au kurudi Yanga nitashukuru Mungu kwa sababu lengo langu ni kucheza mpira ili niweze kufika mbali," alisema straika huyo
Alipoulizwa kama kwa moto huo aliouwasha ameingia kwenye kinyang'anyiro cha ufungaji bora, alijibu ni mapema mno kwa sasa kuongelea hilo
"Kuhusu ufungaji bora, hayo ni mambo ya mbele sana, ila kwa sasa wacha nipambane, kila mechi kwangu ni fainali," alisema
Kabla ya bao hilo, Agosti 17, mwaka huu alifunga bao moja lililoipa ushindi wa 1-0, Mashujaa FC dhidi ya Dodoma Jiji, Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma, likiwa ni bao la kwanza kufungwa msimu huu wa ligi 2024/25
Straika huyo alisajiliwa 2022 na Yanga kutoka Mbeya Kwanza, lakini baada ya kukosa namba, klabu hiyo ilimpeleka Coastal Union kwa mkopo wa mwaka mmoja, ambapo aliumaliza mwishoni mwa msimu uliopita na msimu huu amesajiliwa Mashujaa kama mchezaji huru



