Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amesema maandalizi kuelekea mchezo dhidi ya Simba yamekamilika na wanakwenda kwenye mchezo huo wakiwa na furaha
Gamondi amesema kikosi chake hakikuwa na jambo jipya katika maandalizi kwani mechi dhidi ya Simba haina tofauti na mechi nyingine walizocheza kwenye ligi
"Tuna furaha kubwa kuelekea kwenye ligi huku tukiwa na mchezo muhimu wa Derby. Tupo vizuri, tuna matumaini makubwa ya kufanya vizuri hapo kesho. Hatujabadilika sana kwenye maandalizi tumejiandaa kama ambavyo tumekuwa tukifanya hapo awali:
"Tumetokea kwenye wiki ya FIFA na mara nyingi tunapata changamoto kidogo ya maandalizi kwani wachezaji wetu wengi wanakuwa kwenye majukumu ya timu za TAIFA"
"Kwa mfano kuna wachezaji wamefika jana na wengine wanaingia leo kwa mantiki hiyo lazima upate ugumu kwenye maandalizi lakini tutafanya kila liwezekanalo," alisema Gamondi
Gamondi amesema anatarajia mchezo huo utakuwa mzuri na kuwapa burudani mashabiki watakaojitokeza kushuhudia
"Tunawaheshimu Simba, ni timu nzuri yenye wachezaji na kocha mzuri. Naamini itakuwa mechi nzuri yenye ushindani na kuwapa burudani mashabiki"
"Nafikiri ni jambo zuri kwa soka la Tanzania kuwa na aina ya mechi hii yenye ushindani ambayo naamini itazidi kulitangaza soka la Tanzania," aliongeza Gamondi
Aidha Gamondi amethibitisha kikosi chake kiko kamili na hakuna mchezaji wake muhimu ambaye atakosekana



