Jana Yanga ilijihakikishia ushindi wa nne mfululizo dhidi ya watani zao Simba katika mchezo wa ligi kuu uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa
Bao la kujifunga Simba dakika ya 86 baada ya shuti la Maxi Nzengeli kumgonga Kelvin Kijili, lilitosha kuihakikishia Yanga ushindi wa tano mfululizo katika ligi msimu huu na kupanda hadi nafasi ya pili katika msimamo wa ligi
Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi amedhihirisha ubora wake mbele ya Simba kikosi chake kikiweka rekodi ya kugawa vipigo vinne mfululizo kwa watani
Yanga ilianza mchezo huo taratibu na kuwapa Simba nafasi ya kumiliki mchezo katika dakika 25-30 za kipindi cha kwanza
Gamondi alisema ulikuwa mkakati wao wa kimbinu kuanza hivyo kwa sababu alifahamu Simba wangeanza mchezo huo kwa kasi huku pia kikosi chake kilikabiliwa na changamoto ya uchovu kwa baadhi ya wachezaji waliokuwa katika majukumu ya timu za Taifa
"Baadhi ya wachezaji walifika siku moja kabla ya mchezo na wengine walirudi Alfajiri ya siku ya mchezo, utaona ni kwa kiasi gani tulikuwa na changamoto kubwa katika maandalizi yetu"
"Tulicheza kwa tahadhari kubwa katika kipindi cha kwanza tukifahamu wapinzani wetu wataanza na kasi kubwa lakini kipindi cha pili tulifanya mabadiliko ya kimbinu, tukamiliki mchezo nadhani tulistahili kushinda"
"Nawapongeza wachezaji wangu haikuwa mechi nyepesi, ushindi huu ni matokeo ya ari ya kujituma kwao kwa dakika zote 90 za mchezo," alisema Gamondi
Kuingia kwa Kennedy Musonda, Clement Mzize na Clatous Chama kulibadili taswira ya mchezo ambapo Yanga iliongeza kasi ya mashambulizi kupelekea kupata bao hilo dakika za jiooooooooni



