Meneja wa Habari na Mawasiliano klabu ya Simba Ahmed Ali amesema kupoteza mchezo wa ligi kuu dhidi ya watani zao Yanga hakuwezi kuwatoa katika mipango yao ya kuwania ubingwa msimu huu
Oktoba 19 Simba ilichapwa bao 1-0 na Yanga katika mchezo uliopigwa uwanja wa Benjamin Mkapa, matokeo ambayo ni kama yamewakatisha tamaa mashabiki wa timu hiyo
Ahmed amesema kila Mwanasimba ameumizwa na matokeo hayo lakini wana matumaini katika malengo yao kwa sababu bado safari ni ndefu kukamilisha msimu huu
Msemaji huyo wa Simba amesema licha ya kupoteza mchezo huo, project yao ya kujenga Simba imara imeanza kuonyesha matunda
"Tunaumia kwa kupoteza mchezo wa derby lakini tunajipongeza kwa kuwa mradi wetu wa kutengeneza timu umeanza kutoa matunda tena kwa haraka sana"
"Wote ni mashahidi misimu kadhaa nyuma tulifungwa derby na kuzidiwa kwa dakika zote 90. Tumeona tofauti kubwa, tumefungwa lakini tumeutawala mchezo kwa asilimia kubwa na kama kila kitu kingekua sawa basi tungeshinda mchezo ule"
"Muhimu kwetu wana Simba kwanza tukubali tumepoteza na wala hakuna haja ya kuanza kuhesabu tumepoteza mara ngapi, mpira ni maisha ya duara muda wetu utafika na sisi tutatawala derby kwani tumewahi kufanya hivyo"
"Muhimu kwa sasa ni kusahau yaliyotokea na kujipanga upya kwa vita iliyo mbele yetu. Tumebakiwa na michezo 24 nguvu kubwa iwe kushinda michezo hiyo, tumepoteza derby sio ubingwa," alisema Ahmed
Leo Simba iko mkoani Mbeya kumenyana na Tanzania Prisons katika mchezo mwingine wa ligi kuu ya NBC



