Mlinda lango wa Yanga Djigui Diarra amesema mchezo wa ligi kuu dhidi ya Simba uliopigwa Jumamosi iliyopita katika uwanja wa Benjamin Mkapa, ni moja ya mechi zilizoingia katika kumbukumbu ya maisha yake ya soka katika ardhi ya Tanzania
Yanga iliibuka na ushindi wa bao 1-0 katika mchezo huo ambao Diarra amefichua kuwa alishuka uwanja wa ndege wa Kimataifa Julius Nyerere na moja kwa moja kuelekea uwanja wa Benjamin Mkapa kucheza mchezo huo
"Mechi yangu bora ya Simba na Yanga tangu nifike hapa ni hii ya juzi ya ushindi wa bao 1-0 kwa sababu nilifika Tanzania siku ya mechi"
"Nashukuru sana tuliweza kushinda, kwa kweli hii inabaki kuwa mechi yangu bora sana," alisema Diarra
Diarra amemshukuru Rais wa Yanga kwa kuhakikisha anafanya kila linalowezekana ili awahi mchezo huo akiwa ametoka katika majukumu ya timu ya Taifa ya Mali
"Rais alinitengenezea mazingira mazuri ya usafiri, sikuchoka kwani nilipata tiketi ya Business Class"
"Nilivyotua uwanja wa ndege alituma mtu anifuate ili niwahi moja kwa moja uwanjani. Kama kuna siku niliuwazia ushindi basi ni siku ile," aliongeza Diarra
Akizungumzia tukio la kuinusuru Yanga kufungwa bao la mapema katika mchezo dhidi ya Simba, Diarra alisema amekuwa akiifuatilia Simba katika mechi zao hivyo alikuwa na ufahamu juu ya maamuzi ya mshambuliaji Lionel Ateba
"Huwa naangalia mechi za Simba kwa hiyo nawajua. Nilimuona (Ateba) anavyocheza, nilifahamu akipata mpira eneo lile atafanya nini, nilijua ataenda kushoto na sikuwa na presha"
"Nilivyookoa sikuhama eneo nikasimama vilevile kwani nilijua mpinzani atapiga nikaokoa tena," alisema Diarra



