Mikiki mikiki ya ligi kuu ya NBC inaendelea leo ambapo mechi tatu zinatarajiwa kupigwa katika viwanja mbalimbali
Vinara wa ligi hiyo Singida BS, saa 8 mchana watakuwa uwanja wa nyumbani CCM Liti kuwakaribisha wapinzani wao wakuu Fountain Gate. Hii ni Derby ya mapacha ambayo inapigwa mapema
Hata hivyo Fountain Gate wanakwenda kwenye mchezo huo bila ya huduma ya wachezaji wao mauhimu, Selemani Mwalimu ambaye ni kinara wa ufungaji msimu huu akiwa na mabao 6 na Edgar William ambaye anashika nafasi ya pili akiwa na mabao manne
Wachezaji hao wamejumuishwa kikosi cha timu ya Taifa wachezaji wa ndani kinachotarajiwa kucheza dhidi ya Sudan Oktoba 27
Saa 10:15 jioni mchezo mwingine mkali kati ya Simba dhidi ya Namungo Fc utapigwa katika uwanja wa KMC Complex jijini Dar es salaam
Simba inayoshika nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi itakuwa ikisaka alama tatu ambazo zinaweza kuwasogeza juu ya watani zao Yanga katika msimamo wa ligi
Hata hivyo wanakwenda kukutana na Namungo Fc ambayo juzi ilimtangaza Juma Mgunda kuwa kocha wake mkuu
Mgunda amefanya kazi Simba kwa takribani misimu mitatu hivyo unaweza kusema anawajua vyema waajiri wake hao wa zamani
Saa 1 usiku Azam Fc itakuwa uwanja wa nyumbani, Azam Complex kuumana na KenGold inayoburuza mkia katika msimamo wa ligi




