Kocha Mkuu wa Yanga Miguel Gamondi ameitaka Bodi ya Ligi kuzingatia afya za wachezaji inapoandaa ratiba ya mechi za ligi kuu ya NBC
Gamondi ametoa malalamiko hayo wakati akizungumza katika Mkutano na Wanahabari kuelekea mchezo wa ligi kuu kati ya Coastal Union dhidi ya Yanga utakaopigwa uwanja wa Sheikh Amri Abeid, Jumamosi Oktoba 26
Gamondi amesema hawana muda wa kufanya maandalizi ya mechi na wachezaji kupumzika kwa sababu ratiba inawalazimu kucheza kila baada ya siku tatu
"Wanaoandaa kalenda wanatakiwa wafahamu wachezaji sio maroboti ni binadamu na hata Ulaya tayari wameanza kuilalamika FIFA kuwa na ratiba inayobana mechi nyingi za ligi ya mabingwa na hiyo imeanza na hapa"
"Madhara ya hayo yote ni majeraha kwa wachezaji na italeta athari kwa wachezaji na ubora wa mechi kupungua"
"Tunacheza mechi ambayo wapinzani wetu wanajiaandaa kwa siku 7 mpaka 8 lakini sisi tunafanya mambo ndani ya muda mchache"
"Yasichukuliwe kama malalamiko lakini yawe ni kama maboresho kwa watu wanaoandaa kalenda kwa manufaa ya ligi,"alisema Gamondi
Akizungumzia maandalizi ya kikosi chake kuelekea mchezo huo, Gamondi alisema anatarajia mchezo hautakuwa mwepesi, akihofia uwanja hautawaruhusu kucheza aina yao ya soka
"Tunategemea itakuwa mechi ngumu kwa kuzingatia uwanja pia hauruhusu kucheza aina yetu ya mpira lakini tutajitahidi kufanya kile kinachowezekana na tumekuja hapa tukiwa na malengo ya kushinda mechi," aliongeza Gamondi



