Wekundu wa Msimbazi Simba Sc wameendeleza ubabe wao katika uwanja wa KMC Complex wakiibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Namungo Fc katika mchezo wa ligi kuu ya NBC
Ulikuwa mchezo wa upande mmoja kwa muda mwingi, pengine mambo yangekuwa mabaya zaidi kwa Namungo Fc kama Simba ingetumia vyema nafasi nyingi walizotengeneza
Mabao ya Simba katika mchezo huo yalifungwa na Shomari Kapombe aliyefunga bao la mapema dakika ya 5 kabla ya Jean Charles Ahoua kuongeza la pili dakika ya 33 muda mfupi baada ya kuingia akichukua nafasi ya Awesu Awesu aliyeumia
Ahoua amefikisha mabao matatu akiwa ndiye kinara wa mabao kwa upande wa Simba akiwa pia na pasi nne za mabao
Msumari wa mwisho katika jeneza la Namungo Fc ulipigiliwa na kiungo Debora Mavambo na kuihakikishia Simba alama tatu muhimu zilizowasogeza hadi nafasi ya pili katika msimamo wa ligi
Mambo bado ni magumu kwa Namungo Fc ambayo leo imepoteza mchezo wa tatu mfululizo



