Gamondi alalamikia viwanja ligi kuu

Joel JJ By Joel JJ β€’ 28th October 2024


Gamondi alalamikia viwanja ligi kuu

Kocha Mkuu wa Yanga, Miguel Gamondi, ameulalamikia Uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha, akisema hauko kwenye ubora, huku akisema viwanja vitatu tu vinavyobeba taswira ya soka la Tanzania ni ule wa Benjamin Mkapa, Azam Complex, ambavyo vyote vipo, Dar es Salaam na New Amaan Complex, Zanzibar

Akizungumza baada ya kumalizika kwa mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya timu yake na Coastal Union, akiibuka na ushindi wa bao 1-0 lililowekwa wavuni na Jean Baleke, Gamondi amesema, baadhi ya viwanja ni vibovu kiasi kwamba vinasababisha timu zicheze mpira wa kubutuabutua kitu ambacho si picha nzuri kwa Ligi ya Tanzania

"Pointi hizi tatu ni muhimu sana kwetu katika mwendelezo wa kupigania nafasi ya kutwaa ubingwa, lakini sijafurahishwa na hali ya uwanja, pamoja na baadhi ya maamuzi ya mwamuzi"

"Kwa wachezaji wakubwa na ligi bora huwezi kucheza mpira kwenye uwanja kama huu, haikuwa mbaya kwa upande wetu, hata Coastal Union walikuwa wakipiga mipira mirefu, walijaribu kama mara mbili tatu kuanzia mpira nyuma wakashindwa na kuanza kubutua na hii si picha nzuri kwa Ligi ya Tanzania"

"kwangu mimi, Uwanja wa Azam Copmlex, New Amaan Zanzibar na Benjamin Mkapa, ndivyo vinavyobeba taswira njema ya ligi ya hapa nchini," alisema kocha huyo

Baada ya ushindi huo, Yanga inaelekea Zanzibar kwa ajili ya mchezo mwingine dhidi ya Singida Black Stars utakaopigwa Jumatano Oktoba 30 katika uwanja wa New Amaan Complex


  

XTRA 90 INSIDER

Get the latest tactics & rumors delivered to your inbox.