Msafara wa kikosi cha Yanga umeondoka jijini Dar es salaam mapema leo kuelekea Zanzibar kwa ajili ya mchezo wa ligi kuu dhidi ya Singida Black Stars ambao utapigwa kesho Jumatano, Oktoba 30 katika uwanja wa New Amaan Complex
Wakati Yanga wakielekea Zanzibar leo, wapinzani wao Singida BS wako Zanzibar tangu juzi wakiendelea na maandalizi ya mchezo huo unaosubiriwa kwa hamu na mashabiki wa soka nchini
Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Yanga Ali Kamwe ametamba kuwa wanakwenda Zanzibar kuchukua alama tatu kwani wapinzani wao wamefanya makosa kupeleka mchezo huo Zanzibar ambako ni ngome yao
Kumekuwa na vita ya maneno baina ya wasemaji wa timu hizo Kamwe na Hassan Massanza ambaye jana alitoa tahadhari kuwa hawapaswi kwenda na matokeo yao mfukoni
Mchezo huo unazikutanisha timu mbili zenye rekodi bora katika ligi kuu msimu huu
Singida Black Stars wako kileleni mwa msimamo wa ligi wakikusanya alama 22 baada ya kushinda mechi saba na kutoka sare mchezo mmoja
Yanga inashika nafasi ya pili ikiwa na alama 21 baada ya kucheza mechi saba na kushinda zote pasipo kuruhusu bao
Dakika 90 za mchezo wa kesho zitaamua kama ni Yanga inayokwenda kukaa kileleni kama itaibuka na ushindi au ni Singida BS watakaobaki hapo kama watashinda au hata kutoka sare



